
Watu 18 wamefariki dunia makumi wengine wakijeruhiwa nchini Madagascar baada ya polisi kufyatua risasi ili kutawanya kundi la watu waliokuwa wamekasirishwa kutekwa nyara mtoto mwenye ulemavu wa ngozi au albino.
Kwa mujibu wa shirika la habari la AFP, ripoti hiyo imetolewa na Tango Oscar Toky ambaye ni daktari mkuu kwenye hospitali moja kusini mashariki mwa Madagascar.
Toky ameongeza kuwa kati ya watu 34 waliojeruhiwa, 9 ni mahututi akiongeza kwamba wanasubiri helikopta za serikali kuwapeleka hospitali ya mji mkuu wa nchi hiyo.
Watu wapatao 500 waliokuwa wamebeba visu na mapanga walijaribu kuingia kwa nguvu kwenye kituo cha polisi ambako washukiwa wa utekaji nyara walikuwa wameshikiliwa.
Ofisa wa polisi kutoka mji wa tukio wa Ikongo ulioko takriban kilomita 90 kusini mashariki mwa mji mkuu wa Antananarivo wakati akizungumza kwa njia ya simu na AFP amesema walijaribu kushauriana na waandamanaji hao lakini pale walipokataa kusikia, hawakuwa na njia nyingine ila kutumia risasi za moto ili kujilinda.
Mkuu wa polisi kitaifa Andry Rakotondrazaka amewaambia wanahabari kwamba tukio hilo ni la kuhuzunisha na kwamba lingezuilika.
