
Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta ameomba kikosi cha Kanda ya Afrika Mashariki, kipelekwe eneo la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), lenye mzozo ili kurejesha usalama mashariki mwa nchi hiyo, ambako mapigano makali ya hivi karibuni yamezusha tena uhasama wa zamani.
Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, nchi yenye utajiri wa madini inasumbuka kudhibiti dazeni ya makundi yenye silaha mashariki mwa taifa hilo kubwa, ambayo mengi kati yao ni urithi wa vita viwili vya kikanda vilivyopiganwa robo karne iliyopita.
Ghasia za wiki kadhaa zimechochea mvutano wa kidiplomasia kati ya DRC na jirani yake Rwanda, DRC ikiishtumu kwa uasi wa hivi karibuni wa kundi la waasi wa M23 ulioibuka tena.
Rwanda ilikanusha mara kadhaa kwamba haiwasaidii waasi hao, huku nchi hizo mbili kila moja ikiishtumu nyingine kuendesha mashambulizi ya makombora ya kuvuka mpaka.
“Natoa wito wa kuanzishwa kwa Jeshi la Afrika Mashariki chini ya usimamizi wa Jumuia ya Afrika Mashariki,”, Kenyatta amesema katika taarifa yake.
Ameongeza kuwa “uhasama uliopo” umetishia kukwamisha mchakato wa kisiasa unaoendelea kushughulikia hali ya usalama katika nchi hiyo yenye raia milioni 90.
Uamuzi wa kuunda kikosi cha kikanda ulichukuliwa mwezi Aprili wakati Kenyatta alikuwa mwenyeji wa viongozi wa Uganda, Burundi, Rwanda na DRC mjini Nairobi kujadili mzozo wa DRC.
“Makamanda wa kijeshi wa nchi saba wanachama wa Jumuia ya Afrika mashariki watakutaka Jumapili kukamilisha maandalizi ya kupeleka kikosi hicho cha mseto.
“Jeshi la Kanda ya Afrika Mashariki litapelekwa katika majimbo ya Ituri, Kivu Kaskazini na Kivu Kusini mara moja kuleta utulivu katika eneo hilo na kuimarisha amani.” Kenyatta amesema.
