
Shirika la habari linalomilikiwa na serikali ya Misri limesema Gavana wa Benki Kuu, Tareq Amer, amejiuzulu nafasi hiyo jana Jumatano wakati taifa hilo la kiarabu lenye idadi kubwa ya watu likiendelea kutumbukia kwenye mzozo wa kiuchumi.
Kwa mujibu wa shirika la habari la AFP, rais Abdel Fattah al Sisi amekubali kujiuzulu kwa Amer aliyechukua wadhifa huo 2015, na aliyetarajiwa kuendelea na wadhifa huo hadi mwaka ujao, gazeti la serikali la Al- Ahram limesema.
Sisi hata hivyo amemtaja Amer kuwa mshauri wake, ingawa hakuna taarifa zozote kuhusu ni nani atakayejaza nafasi yake.
Amer anaondoka wakati sarafu ya misri ikiwa kwenye kiwango cha 19.1 dhidi ya dola moja ya Marekani, kikiwa kiwango cha chini zaidi tangu wakati sarafu ya taifa hilo ilipo shushwa thamani wakati wa msimu wa baridi 2016.
Mwezi Machi mwaka huu, Misri pia ilishusha thamani ya sarafu yake kutokana na mfumuko mkubwa wa bei za bidhaa.
Kabla ya vita vya Ukraine, Misri ilikuwa muagizaji mkubwa ulimwenguni wa ngano kutoka Urusi na Ukraine.
Baadhi ya bei za vyakula nchini humo zinasemekana kupanda kwa viwango vya hadi asilimia 66, na hivyo kupelekea thamani ya fedha kushuka kwa hadi asilimia 15. Takriban watu milioni 30 kati ya milioni 103 nchini Misri wanaishi katika hali ya umaskini.
