
Rais wa Marekani Joe Biden amepangwa kuhutubia baraza kuu la Umoja wa Mataifa mjini New York leo Jumatano wakati akitarajia kuangazia juhudi za utawala wake katika kukabiliana na ukosefu wa usalama wa chakula ulimwenguni, kati ya masuala mengine.
Biden pia anatarajiwa kuzungumzia suala la kurejesha mfuko wa kimataifa wa kukabiliana na Ukimwi pamoja na magonjwa mengine, kusawazisha upelekaji bidhaa pamoja na tatizo la mabadiliklo ya hali ya hewa.
Mshauri wa kitaifa wa Marekani wa masuala ya usalama, Jake Sullivan amesema hotuba ya Biden pia itaangazia uchokozi wa Urusi nchini Ukraine.
Ameongeza kusema kwamba atakemea vikali vita hivyo wakati akiomba jumuia ya kimataifa kuendelea kusaidia taifa hilo ambalo limeshambuliwa kwa miezi kadhaa sasa.
Wakati akijubu swali kutoka sauti ya Amerika, Sullivan alisema Biden pia atazungumzia suala la marekebisho kwenye baraza la usalama la Umoja wa Mataifa, ambako Urusi ni mwanachama wa kudumu.
Ijumaa iliyopita balozi wa Marekani kwenye Umoja wa Mataifa, Linda Thomas Greenfield alisema ingawa suala la Ukraine haliwezi kuepukika wakati wa mkutano huo, kuna masuala mengine mengi yatakayozungumziwa pia.
