
Wizara ya mambo ya nje ya Urusi imesema juhudi za nchi za magharibi na mataifa yanayounda kundi la G7 ya kutaka kuitenga Moscow, yamesababisha uhaba mkubwa wa chakula duniani.
Mawaziri wa mambo ya nje wa G7 Jumamosi waliahidi kuimarisha kutengwa kwa Urusi kiuchumi na kisiasa, kuendelea kuipa silaha Ukraine na kufanya kazi pamoja ili kupunguza uhaba wa chakula uliosababishwa na uvamizi wa Urusi Februari 24, dhidi ya jirani yake.
“Majaribio ya kuitenga Urusi kiuchumi, kifedha na upande wa usafirishaji kutoka kwenye njia za muda mrefu za ushirikiano wa kimataifa yanafanya mzozo wa kiuchumi na chakula kuwa mbaya zaidi,” wizara ya mambo ya nje ya Urusi imesema katika tovuti yake.
“Izingatiwe kuwa ni hatua za upande mmoja za nchi za magharibi, hasa kutoka kundi la G7, ambalo limezidisha tatizo la kutotumia tena njia za kawaida za usafirishaji wa bidhaa na mifumo ya fedha kwa ajili ya usambazaji wa chakula kwenye masoko ya dunia,” wizara hiyo imeongeza.
Kabla ya vita, Ukraine na Russia pamoja zilikuwa zinazalisha asilimia 29 ya ngano kwa ajili ya soko la dunia.
